Risala ya kiongozi muadhamu wa mapinduzi ya kiislamu kwa vijana wa ulaya na amerika kaskazini
Transcript of Risala ya kiongozi muadhamu wa mapinduzi ya kiislamu kwa vijana wa ulaya na amerika kaskazini
Risala ya Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu kwa Vijana wa Ulaya na Amerika
Kaskazini
21/01/2015
Bismillahir Rahmanir Rahim
Kwa vijana wote wa Ulaya na Amerika Kaskazini
Matukio ya hivi karibuni ya nchini Ufaransa na
mfano wake katika baadhi ya nchi za Magharibi
yamenifanya niamue kuzungumza nanyi moja
kwa moja kuhusu matukio hayo.
Ninakukhutubuni na kukulengeni nyinyi (vijana)
si kwa sababu ya kutaka kubeba jukumu la wazazi
wenu, hapana bali ni kwa sababu mustakbali ya
mataifa na nchi zenu yamo mikononi mwenu; na
pia ni kwa sababu ninaona shauku na hamu ya
kutafuta ukweli ni kubwa sana katika nyoyo zenu.
Hapa siwalengi viongozi na wanasiasa wenu
kwani ninaamini kuwa wanafanya makusudi kutenganisha njia ya siasa na njia ya ukweli na
uhalisia wa mambo.
Ninapenda kuzungumza nanyi kuhusu Uislamu, hususan kuhusiana na sura ya Uislamu ambayo
inaoneshwa kwenu. Kuna njama nyingi zimefanyika katika kipindi cha zaidi ya miongo miwili
iliyopita, takriban tangu baada ya kusambaratika Umoja wa Kisovieni kwa ajili ya kuifanya dini
tukufu ya Kiislamu kuwa adui mkubwa anayetisha. Kueneza chuki dhidi ya Uislamu na kutumia
vibaya suala hilo, kwa bahati mbaya ni jambo la zamani sana katika hostoria ya kisiasa ya
Magharibi.
Hapa sina nia ya kuonyesha ni vitendo gani vya kueneza chuki vilivyoenezwa kwa mataifa ya
Ulaya hadi hivi sasa. Nyinyi wenyewe kwa kutupia jicho kitogo tu utafiti wa kiukosoaji
uliofanywa hivi karibuni kuhusiana na historia mtaona kuwa katika uandishi mpya wa historia,
kuna miamala na vitendo visivyo vya kiuaminifu na vya upotoshaji vilivyofanywa na tawala za
Magharibi dhidi ya mataifa mengine duniani na dhidi ya tamaduni za mataifa mbali mbali ya
dunia. Historia ya Ulaya na Marekani imejaa mambo ya aibu ya kuwafanya watu watumwa
katika enzi za ukoloni. Historia hiyo imejaa maovu ya aibu kama ya ukatili waliofanyiwa watu
wasio Wazungu na wasio Wakristo. Watafiti na waandishi wenu wa historia wanachanganyikiwa
na wanaemewa na kuingiwa na tahayuri kila wanapoona umwagaji mkubwa wa damu
uliofanyika kwa jina la dini ya Kikristo imma kwa jina la Ukatoliki au Uprotestani au kwa jina la
utaifa na ukabila na kaumu ya taifa fulani na kuwatwisha walimwengu vita vya kwanza na vya
pili vya dunia.
Kuwa na hisia hizo za kuona aibu kwa vitendo hivyo ni jambo la kupongezwa na lengo langu
katika kukumbushia faharasa hiyo ndefu ya maovu yaliyofanywa na nchi za Magharibi si
kuchimbua na kutoa aibu za historia hiyo, bali lengo langu ni kukutakeni muwaulize wasomi
wenu, kwa nini mara zote wananchi wa nchi za Magharibi wanaamka na kujua ukweli baada ya
kupita makumi kadhaa ya miaka na baadhi ya wakati wanaamka baada ya kupita mamia kadhaa
ya miaka? Kwa nini hisia za ndani ya nyoyo za wananchi wa Magharibi mara zote lazima
zitegemee mambo yaliyopita muda mrefu nyuma, si masuala ya sasa hivi? Kwa nini kunawekwa
vizuizi vya kuwafikia inavyotakiwa watu wa Magharibi utambuzi na mambo kuhusu suala
muhimu kama Uislamu na umuhimu wa kuamiliana kwa njia sahihi na utamaduni na tafakuri ya
Kiislamu?
Nyote mnajua vyema kwamba, kujaribu kuidunisha na kueneza chuki na woga dhidi ya wengine
ndiyo mbinu kuu inayotumiwa na watu madhalimu wanaopenda kujinufaisha binafsi. Natumia
fursa hii kukutakeni mjiulize ndani ya nafsi zenu kwamba kwa nini siasa kongwe za kueneza
woga na chuki, hivi sasa zimeongezewa nguvu mno kwa namna isiyo na mfano dhidi ya Uislamu
na dhidi ya Waislamu? Kwa nini muundo wa nguvu duniani hivi sasa unapenda kuiweka
pembeni fikra ya Kiislamu na kuwa mkali kila fikra hiyo inapojitokeza? Kwani kuna kitu gani
kizuri na cha thamani ndani ya Uislamu ambacho kinasumbua mipango ya madola makubwa na
hivi kuna manufaa gani yanayopata madola hayo pale yanapoeneza sura ghalati na isiyo sahihi
kuhusu Uislamu? Hivyo basi ombi langu la kwanza kabisa kwenu ni kufanya uchunguzi na
udadisi kuhusu misukumo na malengo ya kufanyika kampeni kubwa mno ya kuenezwa sura
isiyo sahihi kuhusiana na Uislamu.
Ombi langu la pili ni kwamba katika konesha kwenu radiamali kuhusu wimbi hili kubwa la
kuhukumu mambo bila ya utafiti wa kina na kabla ya kutokea kwake, fanyeni juhudi za kupata
elimu ya moja kwa moja kutoka katika dini yenyewe ya Kiislamu. Mantiki sahihi inahukumu
kwamba mtu anatakiwa ajue udhati na uhalisia wa kitu anachofanywa akiogope na kukaa mbali
nacho.
Mimi sishikilii kwamba mukubaliane na mtazamo wangu au mtazamo mwingine wowote wa
Kiislamu. Hapana, bali ninachosema mimi ni kuwa, msiruhusu jambo hili muhimu na safi na
lenye taathira kubwa katika dunia ya leo lifikishwe kwenu kwa malengo na shabaha zilizojaa
upotofu. Msiruhusu watu wanaofanya mambo kwa kupenda kujionesha na magaidi
wanaotumiwa na madola ya Magharibi ambao wanajifanya ndio wawakilishi wa Uislamu,
kuziteka akili na fikra zenu. Fanyeni juhudi za kuuelewa Uislamu kupitia vyanzo sahihi na
marejeo yake ya awali na ya moja kwa moja. Utafuteni Uislamu kupitia Qur'ani na sira na
maisha ya Mtume wake Mtukufu (rehema za Allah ziwe juu yake na Aal zake). Hapa ninapenda
kukuulizeni, hivi hadi hivi sasa mumewahi kuisoma Qur'ani Tukufu? Je mafundisho ya Mtume
wa Uislamu (rehema Allah ziwe juu yake na Aal zake) na mafundisho yake yaliyojaa
ubinaadamu na maadili mema mumewahi kuyatalii na kuyasoma? Je hadi hivi sasa
mumeshawahi kupata ujumbe wa Uislamu kupitia vyanzo vingine visivyo vyombo vyenu vya
habari? Je hadi hivi sasa imeshakupitikieni kujiuliza vipi dini hii ya Kiislamu na kwa kutumia
misingi na matukufu gani imeweza kuleta ustaarabu mkubwa wa kielimu na kifikra duniani kwa
karne nyingi na kumzawadia mwanadamu wasomi na wanafikra wakubwa?
Ninachopenda kukuombeni ni kwamba msiruhusu njama za kuoneshwa sura mbaya na ovu
kuhusiana na Uislamu kuwa kizuizi katika hisia zenu na kukuzueni kuhukumu mambo
kiuadilifu. Leo hii zana za kisasa za mawasiliano zimevunja mipaka ya kijiografia, hivyo
msiruhusu wakufungeni ndani ya mipaka ya kupandikizwa na isiyo na ukweli. Ijapokuwa mtu
mmoja mmoja hawezi kuziba mapengo yote yaliyopandikizwa kwa muda mrefu sasa, lakini kila
mmoja wenu anaweza kujenga daraja la fikra na insafu kwenye mapengo hayo kwa lengo la
kujielimisha yeye mwenyewe mambo sahihi na vile vile kuwaelimisha watu wanaomzunguka.
Hii ni changamoto iliyowekwa tangu zamani baina ya Uislamu na nyinyi vijana. Ijapokuwa
changamoto hiyo ni kubwa, lakini inaweza kuzusha maswali mapya katika akili zenu
zinazopenda kuchunguza na kudadisi mambo. Kufanya juhudi za kutafuta majibu ya maswali
hayo ni fursa nzuri ya kukuwezesheni kupata uhakika mpya. Hivyo msiipoteze fursa hii ya kuwa
na welewa sahihi na usio wa kuhukumu mambo kinyume na insafu na uadilifu na kabla ya
kutokea kwake kuhusiana na dini tukufu ya Kiislamu. Msipoteze fursa hili ili kwa kuzingatia
kupenda kwenu kujua ukweli na uhakika, pengine vizazi vinavyokuja vikaandika historia ya
miamala ya kipindi hiki baina ya Uislamu na Magharibi, kwa muono wa wazi na hisia nzuri za
ndani ya moyo.
Sayyid Ali Khamenei
1/11/1393 (Hijria Shamsia)
(Januari 21, 2015).